Saturday , 23rd May , 2020

Askari wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji wilayani Ngara mkoani Kagera, Denice Minja ambaye alimwokoa mtoto katika shimo la choo cha shule ya msingi Murgwanza wilayani humo, ameahidi kumlea mtoto huyo katika maisha yake yote.

Askari wa Zimamoto wilayani Ngara, Denice Minja

Akizungumza baada ya kuvishwa cheo kipya rasmi na Kamanda wa Zimamoto mkoa wa Kagera Hamis Dawa, askari huyo amesema kuwa amekwishafanya mazungumzo na mke wake na wote wamekubaliana kumlea, pia amefuatilia idara ya ustawi wa jamii na kuambiwa mtoto akiruhusiwa kutoka hospitali aende kwa ajili ya kupewa fomu ya kujaza ili akabidhiwe. 

Askari huyo amesema aliposikia sauti ya mtoto yeye kama mzazi alihisi uchungu na kuamua kujitoa mhanga kuingia katika shimo hilo lenye urefu wa mita 30 na baada ya kumfikia mtoto huyo mwenye jinsia ya kike alikuta amefungwa mdomo kwa khanga na kuwa hilo linathibitisha kuwa mhusika alilenga kumuua. 

Akimvisha cheo kipya cha Koplo kutoka cha zamani cha Konstebo, kamanda wa Zimamoto na Uokoaji mkoa wa mkoa wa Kagera, Inspekta Hamis Dawa amesema kuwa askari huyo amepandishwa rasmi cheo jana na Kamishna Jenerali wa jeshi hilo, John Masunga kutokana na ujasiri wake wa kuingia katika shimo kumwokoa mtoto huyo.