Tuesday , 16th Mar , 2021

Kocha wa klabu ya Namungo, Hemed Suleiman Morocco amesema maandalizi ya mchezo wao dhidi ya klabu ya Pyramids ya nchini Misri utakaochezwa kesho saa 10:00 jioni Machi 17, 2021 kwenye dimba la mkapa, yamekamilika na watapambania ili kupata alama tatu.

Kocha wa Namungo, Hemed Suleima Morocco.

Akiongea mbele ya Wanahabari asubuhi ya leo tarehe 16 Machi 2021, Morocco amesema “Tunaiheshimu Pyramids, ni timu kubwa. Tunaenda kuikabili tukiwa na malengo ya kupata alama tatu. Hautakuwa mchezo rahisi ila tuko tayari”.

Baada ya kusema hayo, Morocco alithibitisha kumkosa mlinzi wake wa kulia, Haruna Shamte kutokana na mchezaji huyo kuoneshwa kadi nyekundu kwenye mchezo uliopita dhidi ya Raja Casablanca ambao Namungo walipoteza kwa bao 1-0.

Kwa upande wa Nahodha wa Pyramids, Abdallah El Said amesema “Ni mechi ngumu lakini si mara ya kwanza kuja Tanzania, hali ya hewa ni nzuri  kwahiyo tumejipanga kupata ushindi”.

Namungo ipo kundi D ikiwa inashika mkia baada ya kupoteza mchezo wa kwanza, Nkana Red Devils ya nchini Zambia ipo nafasi ya tatu baada na wenyewe kupoteza mchezo wa kwanza, Pyramids nafasi ya pili wakiwa na alama sawa Raja Casablanca anayeongoza kundi.