Thursday , 5th May , 2022

Chama cha Netiboli Tanzania (CHANETA) wametakiwa kutumia vyombo vya habari kujitangaza zaidi ili kuwapata wadhamini watakaosaidia mchezo huo kukua na kurudisha hadhi ya netiboli nchini.

Makamu Mwenyekiti (CHANETA), Shyrose Bhanji .

Rai hiyo imetolewa leo Mei 05, 2022 na  Afisa michezo mkuu wa Baraza la Michezo Taifa na Mwenyekiti wa kamati ya uchaguzi mdogo wa chama hicho Allen Alex, uchaguzi wa kujaza nafasi zilizokuwa wazi baada ya kukamilika kwa uchaguzi Mkuu ulifanyika  Octoba 2021 Jijini Dodoma.

"Watu ni Soko na soko ndilo litasaidia kuwavutia wadhamini na kuufanya mchezo ukue, hawa wamerudi kuvunja rekodi yao, hivyo wasukumeni wafanye kile mnachotaka wakatekeleze yale mnayokusudia kuirudisha hadhi ya netiboli,"alisema Mwenyekiti wa Uchaguzi na kuongoza kuwa;

"Dunia imekua shirikisheni watoto wa kike itakuwa  kivutio  katika kutangaza mchezo kupitia mitandao yao ya kijamii ili dunia itambue uwepo wenu,"alisisitiza.

Matokeo ya uchaguzi  huo nafasi ya Makamu Mwenyekiti Shy Rose Banji ameibuka kidedea kwa kupata kura zote 34 baada ya kumshinda mpinzani wake Dkt Juliana Manyerere ambaye ameambulia patupu.

Wakati Rose Mkisi akiwabwaga wapinzani wake watatu kwa kupata  kura 19 katika nafasi ya Katibu Mkuu ambao ni Jaqline Sikozi aliyepata kura nane, Rahma Kilimba kura saba na Damiani Chonya ambaye hakupata kura.

Naye Makamu Mwenyekiti wa Chama cha Netiboli Tanzania (CHANETA), Shyrose Bhanji amesema wanaandaa mipango kabambe kurejesha hadhi ya mchezo huo nchini hasa katika ushindani katika anga za kimataifa.

Shy -rose alisema watashirikiana na viongozi wenzake kuhakikisha wanashiriki mashindano ya Kimataifa yakiwamo Afrika Mashariki na Kati, Afrika na Kombe la Dunia.

"Tumerejea katika mchezo tunaoufahamu na kazi  yetu ni kupanga mipango itakayowavutia wadau, tutashirikiana katika kurudisha hadhi na heshima ya mchezo huu  kama awali," amesema Shy-rose.