Friday , 17th Jun , 2022

Mkuu wa kimila wa kabila la Maasai walilkuwa wakiishi katika Hifadhi ya Ngorogoro,  Laigwanani Matigoi Tauwo, amemshukuru Mungu kwa kumuongoza Rais Samia Suluhu Hassan kwa maono yake ya kuwapatia makazi bora katika Kijiji cha Msomera kilichopo wilaya ya Handeni Tanga.

Mkuu wa kimila wa kabila la Maasai Laigwanani Matigoi Tauwo

Akishukuru kwa niaba ya wananchi wenzake  wa Ngorogoro ambao wameamua kuhama kwa hiari yao, Laigwanani Tauwo amesema sasa maisha yao yatakuwa ya amani zaidi na yenye maendeleo kuliko huko nyuma kwa kuwa serikali imewapatia nyumba na ardhi kwa ajili ya killimo na ufugaji, pia huduma bora za kijamii kama elimu na afya. 

"Namshukuru sana Mungu kwa kutupa Rais  Mama Samia, leo sisi tunamiliki nyumba jamani, kweli Mungu mkubwa sana, tunaahidi tutaishi vizuri sana na ndugu zetu wa hapa Msomera" amesema Laigwanani Tauwo.

Katika zoezi la kuwapokea wananchi hao walioamua kuhamia Kijiji Cha Msomera ili kupisha shughuli za uhifadhi Ngorongoro, Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe. Balozi Dkt. Pindi Chana, amewakabidhi wananchi hao hati za  ardhi zilizotolewa na Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi.