Monday , 29th Apr , 2024

Aliyekuwa Kocha Mkuu wa Simba SC Abdelhak Benchikha amewaaga rasmi mashabiki na wanachama wa klabu hiyo baada ya kuomba kusitisha mkataba wake na klabu hiyo mnamo Jumapili ya Aprili 28-2024.

Kocha Benchikha ameweka wazi sababu kuu ya kuondoka ndani ya kikosi hicho sababu binafsi za kifamilia na kukanusha taarifa za mitandaoni kuwa chanzo kikubwa ni kushindwa kufuzu kwa timu hiyo kwenda hatua ya nusu fainali ya ligi ya mabingwa barani Afrika kwa msimu 2023-24

“Viongozi hata mimi nilipenda kumaliza msimu huu na kuendelea lakini matatizo ya mke wangu ya kiafya yamekatiza safari na Simba, uwepo wa mbali na familia imekuwa ngumu kwangu na kupelekea kutofanya kazi vizuri na akili kutotulia''amesema Benchikha

Tayari uongozi wa Simba SC umemtangaza Juma Mgunda kuwa kaimu kocha mkuu akisaidiwa na Msaidizi wake Seleman Matola huku Benchikha anaondoka pamoja na wasaidizi wake wawili Kamal Boujnane na Farid Zemit ndani ya miamba hiyo ya Msimbazi