Alhamisi , 30th Jul , 2020

Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) mkoani Mara, inamshikilia mgombea wa nafasi ya Ubunge wa Viti Maalumu, mkoani humo kutoka CCM kwa kutengeneza vitambulisho vya wajumbe feki zaidi ya 40, kwa lengo la kujipatia kura visivyo halali maarufu kama kura za maruhani.

Vitambulisho feki vilivyokamatwa na TAKUKURU

Akizungumzia tukio hilo Mkuu wa TAKUKURU mkoani humo Alex Kuhanda, amesema kuwa mgombea huyo alishirikiana kutengeneza vitambulisho hivyo na kiongozi wa chama hicho wa ngazi ya Mkoa huku wakijua kufanya hivyo ni kinyume cha sheria za nchi na chama hicho kwa ujumla.

Amesema kuwa uchunguzi unaendelea ili kujua kama wajumbe pia walioshiriki katika uchaguzi huo ni halali, kutokana na kuwepo kwa vitambulisho hivyo hewa, ambapo pia wamebaini kuwa baadhi ya vitambulisho hivyo ni hewa na siyo majina ya wajumbe waliokuwemo na wala hawatambuliki.