Jumatano , 20th Nov , 2019

Viongozi wa Umoja wa Makanisa (UMJM), jijini Mwanza, unaoundwa na Mabaraza matatu ya TEC, CCT na CPCT, umeitaka Serikali kuyapitia upya Makanisa mengine ambayo usajili wake haueleweki, ili kuondoa sintofahamu kwa waumini wa madhehebu hayo.

Mkuu wa Wilaya Nyamagana alipofanya ziara kwenye Kanisa la Mfalme Zumaradi.

Hatua hiyo inakuja ikiwa ni siku chache baada ya Kamati ya ulinzi na Usalama Wilaya ya Nyamagana, ikiongozwa na Mkuu wa Wilaya Dkt. Philis Nyimbi, kufungia Kanisa la Mfalme Zumaridi lililopo eneo la Iseni jijini humo ambalo linadaiwa kuendesha Ibada zake kinyume cha sheria na Katiba ya nchi.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Mwanza, Mwenyekiti wa umoja huo, Askofu Philipo Mafuja amesema hatua hiyo iliyofanywa na viongozi wa Serikali kuyafungia Makanisa yanayoendeshwa kinyume cha sheria yanabaraka hata kwa Mungu.

"Maandiko matakatifu yanasema tuilinde imani na kulinda imani ni hii kuyachukulia hatua baadhi ya Makanisa ambayo yanafanya kazi kinyume na utaratibu" amesema Askofu Philipo Mafuja

Novemba 18, 2019 Uongozi wa Wilaya ya Nyamagana Mkoani Mwanza umepiga marufuku ibada zinazoendeshwa na kiongozi wa kanisa la Mfalme Zumaridi hadi hapo Serikali itakapojiridhisha kuwa ibada hazikinzani na sheria za nchi.