Jumatano , 15th Apr , 2015

Tume ya Taifa ya Uchaguzi nchini Tanzania itaanza kusambaza mashine za BVR 248 katika mikoa minne nchini Tanzania kuanzia katikati mwa wiki ijayo ili kuanza kujiandikisha katika daftari la kudumu la mpiga kura.

BVR zikiwa tayari kwa ajili ya kuanza kusambazwa kwenye mikoani.

Mkuu wa kitengo cha Ufundi wa idara ya Daftrari/ICT wa NEC Dk Sisit Karia, amesema mikoa iliyoanza kupokea mashine hizi ni Lindi, Mtwara, Ruvuma, Iringa na kwamba mpaka sasa wananchi wa mikoa ya Lindi, Mtwara, Ruvuma na Iringa wakae tayari kwani muda wowote watatangaziwa vituo vya kujiandikisha.

Mikoa zitakakopelekwa katika awamu ya pili ni Katavi, Mbeya, Dodoma, Singida Tabora Geita na Kigoma.

Pamoja na mshine hizo 248 Tume ya taifa ya uchaguzi imewaandaa wataalamu 248 ambao watakuwa na jukumu la kutoa elimu kwa wataalamu wengine 50 kwa kila mmoja nchi nzima kwa ajili ya kuharakisha uandikishaji kwa mfumo wa BVR.

Dk Sisit ameeleza kwamba wamefanikiwa kufanya maboresho makubwa katika mashine hizi ikiwa ni pamoja na kubadilisha upangaji wa vifaa (settings), mfumo endeshi (software) na upande wa vichapishio (printers) ambazo sasa zimetengenezewa nchini Ufaransa umeboreshwa na ni rahisi kusafishwa.

Mafunzo yaliyoendeshwa hapa Jijini Dar es Salaam yamechukua siku moja na yamezingatia sana upande wa vichapishio (printers), visoma alama za vidole (Finger Print Scanner) na kamera kutambua macho.

Ameongoza kwamba printer za sasa ni rahisi kusafishwa na hata kuweka kifaa kipya baada ya cha zamani kuharibika vimerahisishwa.

Kuhusu uchukuaji wa alama za vidole, amesema kwa sasa tatizo la mashine ya kuchukua alama za vidole wamelitatua kwa asilimia mia, kwani kwa wale ambao hawana alama za vidole mashine zimewekewa mfumo wa algorithm mpya ambao utatambua kila aina ya kidole.

Pia, kamera zimewekewa mfumo mpya wa kutambua macho mekundu na kurekebisha rangi ya macho mekundu (Red eyes) bila kukwamisha zoezi la uandikishaji.

Mtarajio ni kwamba zoezi la uandikishaji liwe limekamilika ndani ya kila siku 28 tokea kila mkoa unapopokea mashine hizi. Vile vile Dk Sisit ameishukuru serikali kwa kufanikisha upatikanaji wa vifaa, “serekali imejitahidi kuandaa upatikanaji wa mashine hizo, na usafirishaji kwa njia ya ndege kwenda nchi nzima. Kila halmashauri na mkoa utachukua angalau siku 28 kukamilisha mkoa utakapo pokea vifaa,” Dr Sisit amesema.

Mwisho amesema kwamba mashine nyingine 1,600 zitawasili wakati wowote. Serikali imetoa Dola za Kimarekani milioni 72 (Sh. bilioni 133). Kuwasili kwa mashine hizo, kunaifanya NEC kupokea mashine 2,098, huku ikisubiri mashine 5,902, ili kukamilisha 8,000 zinazotakiwa.

Alisema vifaa hivyo vinanunuliwa na serikali kupitia kampuni ya Lithotech Export ya Afrika Kusini, ambayo imeingia mkataba na NEC na inaviagiza kutoka China.