Jumatatu , 3rd Dec , 2018

Chama cha Mapinduzi (CCM) kimetoa msimamo wake dhidi ya vita ya maneno inayoendelea kati ya Katibu Mkuu wa chama hicho, Dkt. Bashiru Ally na aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe.

Humphrey Polepole.

Taarifa iliyotolewa leo jioni Desemba 3, 2018 na Katibu wa Itikadi na Uenezi (CCM), Humphrey Polepole inaeleza kuwa kauli ya Bashiru kumtaka Membe ambaye ni mwanachama wa chama hicho kufika ofisini kwake ni ya kawaida ndani ya CCM.

CCM inapenda kuwafahamisha kuwa imefuatilia kwa ukaribu mjadala unaoendelea kwenye mitandao ya kijamii kuhusu wito alioutoa Bashiru kwa Membe,” imeeleza taarifa hiyo.

Aidha imeongeza kuwa, “Ni kama sehemu ya utaratibu wa kawaida wa Katibu Mkuu kukutana na viongozi na wanachama wa CCM katika kuendelea kuimarisha umoja na mshikamano wa wanachama".

Chama hicho pia kimeeleza ushindi wake ilioupata katika uchaguzi mdogo wa udiwani kwenye Kata 47 Tanzania Bara uliofanyika Desemba 2, 2018, amesema CCM imepita bila kupingwa katika Kata 41 na katika Kata 6 ambako kumefanyika uchaguzi chama hicho kimeshinda kwa kishindo.

Katibu Mkuu wa CCM, Dkt. Bashiru Ally na aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe.

Polepole ameongeza kuwa Desemba 17, chama kitakuwa na kikao cha Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa huku Desemba 18, kitafanyika kikao cha Halmashauri Kuu ya Taifa.

Katika taarifa hiyo Polepole amesema CCM inawataka Watanzania kuendelea kuwa na umoja, mshikamano na upendo katika kipindi hiki ambacho Rais John Magufuli anaendelea kuongoza nchi katika mageuzi ya uchumi na maendeleo.