Alhamisi , 19th Mar , 2020

Idadi ya wagonjwa walioambukizwa na Virusi hatari vya Corona nchini Tanzania imeongezeka na kufikia Sita, ambao wote wawili ni Watanzania waliokuwa wamesafiri kwenda nchi za nje mwezi huu.

Waziri wa Afya Ummy Mwalimu

Taarifa hiyo imetolewa leo Machi 19, 2020, na Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu, na kusema kuwa tayari wagonjwa hao wametengwa na hali zao zinaendelea vizuri.

"Wagonjwa wapya wawili wamethibitika Jijini Dar es Salaam, wa kwanza ni mwanaume (40), aliyesafiri nchi za Uswisi, Denmark na Ufaransa na alirudi nchini Machi 14, mwingine ni mwanaume (40), ambaye alikuwa Afrika Kusini kuanzia Machi 14, na alirejea nchini Machi 17" amesema Waziri Ummy.

Aidha taarifa hiyo imeeleza kuwa juhudi za kuwafuatilia waliokuwa karibu nao zinaendelea, ambapo hadi sasa jumla ya watu 46 wanafuatiliwa jijini Arusha na watu 66 wanafuatiliwa jijini Dar es Salaam.