Jumamosi , 12th Sep , 2015

Serikali imetwaa Ekari 7000 baada ya ubatilishwaji wa Mashamba ya Tanzania Plantation Limited yaliyokuwa yakimilikiwa na mwekezaji kutoka nje, mashamba hayo yanatajiwa kugawanywa kwa wananchi 2000 wenye uhitaji wa ardhi ya makazi na mashamba.

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe. William Lukuvi

Aidha baada ya ubatilishwaji wa mashamba hayo Arusha imepata ekari 6176.5 na Halmashauri ya Meru ekari 925 hivyo kufikia ekari 7101 ambazo zitagawanywa kwa wananchi.

Hayo yameelezwa na Waziri wa Ardhi Nyumba na Makazi, Wiliam Lukuvi wakati akitoa taarifa ya usuluhishi wa migogoro ya ardhi katika mikoa ya Arusha na Manyara katika mkutano wake na waandishi wa Habari, Lukuvi amesema kuwa mashamba hayo yalikuwa na migogoro kwa kipindi kirefu kati ya mwekezaji na wananchi hivyo kutokana na uhitaji mkubwa wa ardhi serikali imeamua kubatilisha mashamba hayo.

Mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya ya Arusha, Fidelis Lumato amesema kuwa ugawanywaji wa mashamba hayo utasaidia kupunguza migogoro mikubwa ya ardhi iliyokuwa inaikabili wilaya hiyo kutokana na uhaba mkubwa wa ardhi.

Mwenyekiti wa eneo la Oljoro Bwana John Molel amesema kuwa shamba la Imani Estate lilikiaa kwa muda wa miaka 12 bila kutumika na mwekezaji hali iliyowalazimu wananchi kujigawia mashamba hivyo kwa mwekezaji kutoa ekari 100 kwa ajili ya wananchi kutapunguza na kuondoa migogoro ya ardhi.

Jumla ya migogoro 80 iliyowasilishwa kwa waziri Lukuvi kutoka katika Halmashauri ya Jiji la Arusha, Halmashauri ya Wilaya ya Arusha na Halmashauri ya Meru imepatiwa ufumbuzi hivyo kupunguza migogoro ya ardhi iliyokuwa ikilisakama jiji la Arusha.