Alhamisi , 21st Mei , 2015

Serikali imesema kuwa kwa kipindi cha miaka mitatu wadau wa maendeleo wamekuwa hawatoi fedha kwa kiasi chote wanachoahidi kitu ambacho kinafanya miradi mingi kukwama.

Waziri Mkuu wa Tanzania Mh. Mizengo Pinda akisisitiza Jambo Bungeni Mjini Dodoma.

Akijibu swali la mbunge wa Kigoma Chuma Mh. David Kafulila leo katika kipindi cha maswali kwa papo kwa hapo, waziri mkuu Mh. Mizengo Pinda amesema wahisani wamekuwa hawatoi fedha hizo kwa muda mrefu na sio kutokana na sakata la Escrow peke yake.

Waziri Pinda amesema kutokana na hali hiyo serikali imeamua kuchukua hatua ya kutengeneza bajeti ambayo itatokana na makusanyo ya ndani ili kuepuka serikali kukwamisha kufanya maendeleo kwa kusubiri fedha za wahisani.

Waziri mkuu ameongeza kuwa sakata la Escrow limeoneka ndiyo sababu ya wahisani kuzuia misaada yao lakini hiyo ni sababu iliyokuja baadaye baada ya kuibuka suala hilo lakini wamekuwa hawatoi fedha kwa kipindi cha karibu miaka miwili mitatu.

Aidha waziri Pinda amemtaka waziri wa fedha atoe kauli ya serikali juu hatua walizochukua baada ya kubainika kuwa kauli yake ya kuwa serikali imeshasaini mkataba wa MCC si ya kweli.