Jumanne , 10th Mei , 2016

Mbunge wa Jimbo la Bunda Mjini kupitia CHADEMA Ester Bulaya ameeleza bungeni kilio cha wananchi wa Bunda ambao wamepitiwa na mradi wa Nyabehu unaotoa maji kutoka ziwa Victoria kwamba wananchi waliopitiwa na mradi huo hawapati maji kwa miaka mingi.

Bulaya ameyasema hayo leo Bungeni Mjini Dodoma wakati akiuliza swali la nyongeza katika wizara ya Maji na Umwagiliaji kuhusiana na kero ya maji jimboni Bunda.

Akijibu swali hilo Naibu waziri wa maji Isack Kamwelwe amesema kwamba serikali inatambua kero ya maji wanayokabiliana nayo wananchi wa Bunda hivyo bajeti ya mwaka 2016 & 2017 itakapopitishwa wananchi wa Bunda watapewa kipaumbele ili kuhakikisha mradi huo wa maji unakamilika ili wananchi hao waweze kunufaika na maji hayo.

Aidha Naibu waziri wa maji na umwagiliaji amewataka wabunge kuhakikisha bajeti ya maji na umwagiliaji inapitishwa bungeni ili matatizo ya maji yaliyopo katika maeneo yao yakaweze kutatuliwa kwa wakati.