Jumatano , 13th Jan , 2021

Jeshi la Polisi mkoa wa Tanga, linamshikilia Simon Pasian Tarimo, mwenye umri wa miaka 37, dereva na mkazi wa Kimara jijini Dar es Salaam, akisafirisha mirungi bunda 1,685 sawa na kilogramu 133, akiwa ameweka kwenye jokofu linalotumika kuhifadhia jeneza lenye maiti wakati wa kusafirisha.

Kamanda wa Polisi mkoa wa Tanga, Blasius Chatanda, akionesha gari lililokamatwa na mirungi

Taarifa hiyo imetolewa na Kamanda wa Polisi mkoa wa Tanga, Blasius Chatanda, na kusema kuwa mtuhumiwa huyo alikamatwa majira ya saa 2:00 usiku huko katika Kijiji cha Manga, Kata ya Mkata, Tarafa ya Mazingara wilayani Handeni mkoani Tanga, ambapo mirungi hiyo ilikuwa ikisafirishwa kutoka Usangi kupelekwa Dar es Salaam, ikiwa imehifadhiwa kwenye gari maalumu la kubebea maiti.

"Mbinu iliyotumika ni kuweka mifuko kwenye jokofu linalotumika kuhifadhia jeneza lenye maiti wakati wa kusafirisha, kitendo ambacho ni kinyume cha matumizi ya gari hilo", amesema Kamanda Chatanda.