Jumanne , 12th Apr , 2016

Hospitali ya rufaa ya Mtakatifu Benedicto Ndanda, ya wilayani Masasi Mkoani Mtwara, inatarajia kuanza kutoa huduma bure za matibabu kwa akina mama wajawazito kuanzia Julai Mosi mwaka huu.

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Mh. Ummy Mwalimu.

Mganga Mkuu wa hospitali hiyo, dkt. Crispin Sapuli, amesema hatua hiyo imetokana na maazimio yaliyofikiwa baina ya kamati ya uendeshaji ya hospitali hiyo na idara ya afya ya halmashauri ya wilaya ya Masasi, ambapo azimio lingine lilikuwa ni kuhudumia wananchi kwa Mfuko wa Afya ya Jamii (CHF).

Aidha, ameiomba serikali kuiongezea ruzuku ya mishahara hospitali hiyo kutokana na gharama za uendeshaji kuongezeka mwaka hadi mwaka huku ikitakiwa kutoa misamaha ya gharama za matibabu kwa makundi maalumu wakiwamo watoto wa umri chini ya miaka mitano.

Serikali kupitia mkopo wa benki ya dunia inajenga maabara ya kisasa hospitalini hapo itakayokuwa ya rufaa, na kutoa huduma za upimaji wa magonjwa mbalimbali hususani ya milipuko, TB na magonjwa mengine ya kuambukiza.