Jumanne , 27th Oct , 2020

Mkuu wa Jeshi la Polisi Tanzania, IGP Simon Sirro, amewataka kujitokeza kwa wingi ili kuchagua viongozi wanaowahitaji katika hali ya amani na utulivu bila uvunjifu wa amani.

Mkuu wa Jeshi la Polisi Tanzania, IGP Simon Sirro.

IGP Sirro ametoa rai hiyo leo wakati akizungumza na vyombo vya habari jijini Dar es salaam, ambapo amemtaka kila mmoja atimize wajibu wake, Tume ya Taifa ya Uchaguzi itimize wajibu wake, mawakala watimize wajibu wao, wagombea watimize wajibu wao na jeshi la polisi litatimiza wajibu wao wa kuhakikisha ulinzi na usalama kwa kila Mtanzania.

Wananchi mjitokeze kwa wingi kupiga kura, na ukimaliza kupiga kura rudi nyumbani kulinda kura sio kazi yako, kura zitalindwa na mawakala waliopelekwa na vyama vyao katika vituo husika, mikusanyiko isiyokuwa ya lazima haitakiwi”, amesema IGP Sirro.

Ameongeza kuwa, “Kuna maisha baada ya uchaguzi, tujihadhari na mihemko isiyokuwa na tija kwa taifa kila mmoja anategemewa na familia yake usipeleke matatizo kwa familia yako, jana usiku Pemba wakati tunasambaza masanduku ya kupigia kura walianza kurusha mawe, kwahiyo hatutarajii hayo kujirudia kama unajua hutopiga kura usiwe sehemu ya kuanzisha vurugu”.