Ijumaa , 6th Nov , 2015

Rais mstaafu wa awamu ya nne Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete ametoa msamaha kwa wafungwa 4160 ikiwa ni muda mfupi kabla ya kuaga na kumpisha mrithi wake Rais Dkt. John Magufuli.

Rais Mstaafu wa awamu ya nne Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete akiwapungua Mkono waliojitokeza katika uwanja wa Uhuru

Taarifa iliyotolewa na waziri wa mambo ya ndani ya nchi, Mathius Chikawe ilieleza kuwa Dkt. Kikwete alitumia madaraka aliyopewa chini ya ibara ya 45(1)(d) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Kati ya wafungwa hao 864 wameachiwa huru na 3293 kupunguziwa kifungo na kubaki gerezani wakitumikia sehemu iliyobaki ya kifungo chao.

Taarifa inasema wafungwa wote wapunguziwe moja ya sita ya vifungo vyao zaidi ya punguzo la kawaida linalotolewa chini ya kifungu 49(1) cha sheria ya Magereza sura ya 58.

Pia taarifa hiyo ilieleza kuwa msamaha huo utawahusu wafungwa wenye matatizo ikiwemo wenye upungufu wa Kinga mwilini, kifua Kikuu, Saratani ambao wapo katika hali mbaya na kuthibitishwa na jopo la Madaktari.

Kundi lingine la msamaha litawahusu wafungwa wa kike walioingia gerezani wakiwa wajawazito pamoja na wanawake walioingia gerezani na watoto na watoto wanaonyonya na wasionyonya.