Jumanne , 10th Feb , 2015

Raisi wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Dk Jakaya Kikwete amezindua jengo la upasuaji na kuweka jiwe la msingi katika jengo la mama na mtoto katika hospitali ya rufaa ya mkoa wa kilimanjaro mawenzi.

Serikali imesema iko katika  hatua za mwisho za kuboresha vituo vya afya vya wilaya na zahanati nchini, kwa kuvipatia vitendea kazi na wataalamu wakiwamo madaktari na wauguzi ili kusogeza huduma za afya  vijijini na hivyo kupunguza vifo vya  mama na mtoto ifikapo mwaka 2017.

Raisi wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Dk Jakaya Kikwete ameyasema hayo wakati akizindua jengo la upasuaji na kuweka jiwe la msingi katika jengo la mama na mtoto katika hospitali ya rufaa ya mkoa wa kilimanjaro mawenzi

Amesema serikali imedhamiria kusogeza huduma za afya katika maeneo mbalimbali nchini hususani maeneo ya vijijini  ili kuhakikisha wanawake wajawazito wanaojifungulia kwenye mikono salama ya wahudumu wa afya ili kupunguza vifo vya mama na mtoto.

Kwa upande wake naibu waziri wa afya Steven Kebwe amesema vifo vya mama na mtoto hapa nchini vimepungua kutokana na idadi kubwa ya wajawazito kuhudhuria kliniki ambapo kwa mkoa wa kilimanjaro asilimia 90 ya wajawazito wanajifungulia katika vituo vya afya.

Naye mkuu wa mkoa wa Kilimanjaro Leonidas Gama na mganga mkuu wa mkoa  Andreleone Quarter wamesema kufunguliwa kwa jengo hilo  la upasuaji ambalo lilikuwa limefungwa kwa zaidi ya miaka mitano kutapunguza adha kwa wagonjwa kwenda katika hospitali za binafsi kutafuta huduma ya upasuaji.