Jumanne , 12th Jan , 2021

Waziri wa Viwanda na Biashara, Geoffrey Mwambe, amewahakikishia wananchi kuwa hali ya upatikanaji wa mafuta ya kula itatengemaa mara baada ya kuanza upakuaji wa mafuta ya kula yanayoingizwa kutoka nje ya nchi kupitia bandari ya Dar es Salaam.

Mafuta ya kula

Changamoto ya uhaba wa mafuta ya kula imetokana na upungufu wa uzalishaji na kutegemea uagizaji wa mafuta ya kula nje ya nchi, bei ya mafuta ya kula hutegemea soko la bidhaa hiyo kulingana na msimu na mabadiliko ya bei ya bidhaa hiyo katika soko la Dunia.

Waziri Mwambe ameongeza kuwa, serikali imezipatia leseni kampuni mbili za uagizaji wa mafuta ya kula ambazo ni East Coast Oil and Fats Ltd na Murzah Wilmar East Africa Ltd, ambazo zimekuwa zikiingiza mafuta ya kula nchini ili kukidhi upungufu wa tani 365,000 MT kwa mwaka ya mahitaji halisi ya mafuta hayo ya tani 570,000 MT kwa mwaka wakati kiasi kinachozalishwa nchini ni tani 205,000 MT kwa mwaka.
 
Aidha, meli mbili zimeingia bandari ya Dar es Salaam na kiasi cha mafuta ya kula yenye ujazo wa 21,800 MT kimepakuliwa katika meli hiyo na sasa kiko tayari kuingia sokoni, na nyingine imetia nanga alfajiri ya Januari 5, 2021, katika Bandari ya Dar es Salaam na ratiba ya ushushaji wa shehena inaonesha kuwa ni Januari 19, 2021 hadi Januari 22, 2021.

Wizara kwa kushirikiana na Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi inaharakisha ushushaji wa mafuta ya kula yanayoingia kutoka nje ya nchi kupitia bandari ya Dar es Salaam ili kuharakisha upatikanaji wa mafuta kwa wananchi na kupunguza kupanda kwa bei.

Pamoja na hayo Wizara imewekeza nguvu katika mkoa wa Kigoma kupitia agizo la Waziri Mkuu kuhusu ushiriki wa taasisi za umma katika uzalishaji wa mchikichi kwa ajili ya usindikaji wa mafuta ya kula.