Jumanne , 19th Jan , 2016

Tatizo la mfumo wa upatikanaji wa ardhi limeendelea kulalamikiwa kuwa tatizo linalofanya kukwamisha shughuli za uwekezaji katika maeneo mbalimbali nchini hususani mkoani Lindi.

Mkuu wa mkoa wa Lindi Jordan Rugimbana

Hayo yamebanishwa na mwakilishi wa mwekezaji kutoka nchini Ufaransa wa kampuni ya Cassava Starch of Tanzania Corporation LTD,.ambao wameshindwa kufanyia kazi azma yao ya kuanzisha kiwanda cha kutengeneza wanga katika eneo la Mtama, kitakachokwenda sambamba na ulimaji na ununuzi wa zao la mhogo ikiwemo kutoka kwa wakulima, kwa madai kwamba hali hiyo inasababishwa na mlolongo mrefu wa mfumo wa upatikanaji wa ardhi,

Akitolea ufafanuzi suala hilo mkuu wa mkoa wa Lindi Jordan Rugimbana, amekiri mfumo uliopo kukwamisha hali hiyo ingawa maeneo mengi yapo wazi kwa shughuli za kilimo na uwekezaji na kwamba kwa sasa ameanza kufanyia kazi hali hiyo kwa kuwatambua wawekezaji wote waliopo katika mkoa wake na kujua mahitaji yao na kile wanachofanya ambapo zoezi hilo la kuwapatia maeneo litawashirikisha wananchi.

Takwimu zinaonesha mkoa huo una eneo kubwa la ardhi ambalo linafaa kwa shughuli za kilimo lakini halitumiki,huku watafiti wakiwa tayari wamewawezesha kupata mbegu bora za aina mbalimbali kwa ajili ya kilimo cha mhogo.

Nao baadhi ya wananchi wa Mtama wilayani Lindi wameziomba mamlaka husika, kuhakikisha wawekezaji hao wanapata eneo la ukubwa wa hekta 6000 kama walivyoomba ili waanzishe kiwanda hicho cha kutengeneza wanga na wao waweze kunufaika kiuchumi na fursa mbalimbali zikiwemo za ajira na maendeleo mengine.