Jumanne , 31st Aug , 2021

Nyumba mbili zenye jumla ya vyumba 17 zilizopo katika kambi ya wavuvi ya Igabiro kata ya Kaagya, Tarafa ya Bugabo, Bukoba mkoani Kagera zimeteketea kwa moto pamoja na mali zote zilizokuwemo katika nyumba hizo.

Picha ya eneo lililoteketea kwa moto

Moto unadaiwa kutokana na mafuta ya petroli yaliyokuwa yamehifadhiwa katika nyumba kulipuka.

Kaimu mkuu wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji wilaya ya Bukoba, Abdulahiman Ngaugia amesema kuwa walipata taarifa za nyumba hizo mali ya Abduswamadu Kalokola na Frederick Mtoka kuteketea kwa moto jana saa 11:30 jioni na kuwahi eneo la tukio, na kufanikiwa kupunguza madhara kwa kuzima moto huo kabla haujaenea zaidi, katika nyumba nyingine.

Kufuatia tukio hilo ambalo mbali na kuteketeza mali halikusababisha kifo au majeruhi, jeshi la zimamoto na uokoaji baada ya kuzima moto huo, walitoa elimu kwa wakazi wa eneo hilo na kuwataka kuchukua tahadhari ili kupunguza ajali za moto.