Jumanne , 12th Apr , 2016

WAZIRI Mkuu wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Kassim Majaliwa ameipongeza timu ya mpira wa miguu ya Namungo FC na kuikabidhi zawadi ya sh. milioni 5 baada ya kuibuka mabingwa wa ligi daraja la tatu mkoa wa Lindi.

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akiwa katika picha ya pamoja na mabingwa wa soka wa Mkoa wa Lindi , timu ya Namungo FC ya Ruangwa baada ya kukabidhiwa kombe.

Ubingwa huo wa mkoa ulionyakuliwa na timu ya wilaya ya Ruangwa, umeiwezesha kupanda daraja la pili taifa, hivyo kupata tiketi ya kushiriki mashindano ya ligi daraja la pili mechi zitakazochezwa nyumbani na ugenini.

Timu hiyo iliyoanzishwa na wafanyakazi wa mgodi wa Green Ganet uliopo Namungo, kijiji cha Chingumbwa wilayani Ruangwa mwaka huu imekuwa mabingwa wa ligi daraja la tatu mkoa wa Lindi hivyo kupata tiketi ya kucheza ligi daraja la pili ngazi ya taifa.

Akipokea kombe hilo jana Waziri Mkuu, Majaliwa amesema amefurahishwa na ubingwa huo, ambapo amewataka wadau wa soka wilayani hapa kuiunga mkono timu hiyo na kuhakikisha inapanda daraja na kucheza ligu kuu ya Tanzania bara.

Pia amesema atafanya mazungumzo na halmashauri kuona kama wanaeneo kwa ajili ya kujenga kiwanja cha mpira wa miguu na litakapopatikana wananchi wanaweza kuanza kujenga mabanda ya biashara kuzunguka kiwanja hicho na kisha kutafuta mfadhili kwa ajili ya ujenzi wa eneo la kuchezea.

Kwa upande wake Shanel Nchimbi, ambaye ni mmoja wa viongozi wa timu hiyo alimuomba Waziri Mkuu, Majaliwa kuisaidia timu hiyo katika utatuzi wa changamoto mbalimbali zinazowakabili ikiwemo ya ukosefu wa kiwanja, vifaa vya michezo na vya huduma ya kwanza, usafiri na daktari.

Nchimbi amesema changamoto ya ukosefu wa uwanja ilisababisha kuutumia uwanja wa michezo wa Sokoine wa wilaya ya Nachingwea kuwa wa nyumbani hivyo kusababisha timu hiyo kutumia gharama kubwa kufika eneo la michezo.