Alhamisi , 22nd Nov , 2018

Pamoja na umuhimu wa maji kwa afya ya binadmu lakini huduma hiyo hairuhusiwi kupatika kupitia kwa mtu kuchimba tu kisima bila kuhusisha mamlaka husika kwaajili ya kupewa maelekezo juu ya eneo sahihi la kuchimba kisima.

Kisima

Hayo yameelezwa na Mwanasheria wa Bonde la Mto Ruvu/Wami,  Bi. Monica Shiwu kwenye MJADALA wa East Africa Television leo Novemba 22, 2018, ambaye amesema kuwa kwa upande wa kanda ya Dar es salaam ili mtu amiliki kisima cha maji ni lazima afike ofisi za Maji Ubungo ili apate usajili pamoja na kupewa mtalaam atakayesimamia zoezi hilo.

''Ni kosa kwa mtu tu kuchimba kisima kiholela ni lazima azione mamlaka aweze kulipia na kupata mtalaam ambaye atamwelekeza ni wapi eneo zuri la kuchimba kisima hususani kwenye maeneo ya makazi ambayo yana shughuli nyingi za binadamu'', amesema.

Aidha amesema kuwa kwa Kisima cha matumizi ya nyumbani mmiliki anatakiwa kulipia shilingi elfu 60,000/= na kwa matumizi ya viwandani ni shilingi laki mbili na hamsini 250,000/=.

Bi. Monica amesisitiza kuwa ni muhimu kwa wananchi kufuata utaratibu huo kwani inasaidia kuondoa magonjwa mbalimbali yatokanayo na wananchi kuchimba kwa mazoea ambapo wengi hujikuta visima vinakuwa hata kwenye mikondo ya vyoo.