Jumatatu , 21st Sep , 2015

Mgombea urais wa Chama cha Mapinduzi CCM, Mh. John Pombe Magufuli amewataka watanzania kuendelea kuhubiri amani popote walipo kwa kuwa nchi bila amani haiwezi kuwa na maendeleo yoyote.

Mgombea wa Urais kupitia CCM Dk. John Pombe Magufuli akihutubia wakazi wa Chato kwenye mkutano wa kampeni za CCM.

Akizungumza wilayani Chato Mkoani Geita Mh. Magufuli amesema tangu utawala wa Mwalimu na viongozi waliofuata waliweza kuweka misingi ambayo inasimamia amani kitu ambacho mpaka sasa watanzania wanajivunia.

Aidha Mh. Magufuli ameongeza kuwa nchi isiyokua na amani kamwe hawezi kufanya maendeleo hivyo ameahidi kuendelea kuhubiri amani katika kipindi chote cha kampeni zake ili kuendeleza misingi iliyojengwa na viongozi waliopita.

Pia Mh. Magufuli ameongeza kuwa watanzani wawabeze watu wanaosema kuwa Tangu Uhuru CCM, haijafanya maendeleo yoyote wakati mpaka sasa miundombinu mingi imejengwa na uchumi wa nchi umeongezeka.

Akitolea mfano wa Chato amesema miaka kumi iliyopita ilikuwa ni kijiji na sasa ni wilaya ambayo kwa kiasi kikubwa imeweza kundokana na nyumba za nyasi pamoja na barabara zake kupitika muda wote.