Jumatatu , 27th Mei , 2019

Aliyekuwa Mbunge wa Singida Kaskazini, Lazaro Nyalandu amekamatwa na TAKUKURU akiwa anasimamia uchaguzi wa kata wa CHADEMA mkoani Singida.

Aliyekuwa Mbunge wa Singida Kaskazini, Lazaro Nyalandu.

Akizungumza na www.eatv.tv Mkurugenzi wa Itikadi na Uenezi wa chama hicho, John Mrema, amethibitisha tukio hilo na kusema kuwa Nyalandu amechukuliwa akiwa kwenye kikao cha chama cha ndani.

"Nyalandu alikuwa kwenye kikao cha ndani ili kuhamasisha uchaguzi wa ndani wa chama, na awali alichukuliwa na polisi hivyo tumewatuma mawakili wetu tayari kufuatilia juu hilo", amesema Mrema.

Taarifa za awali zilidai kuwa, Nyalandu amekamatwa na kuchukuliwa na watu waliokataa kujitambulisha akiwa kwenye kikao cha ndani cha CHADEMA kwenye kata ya Itaja, wilaya ya Singida vijijini mkoani Singida.