Ijumaa , 8th Nov , 2019

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Ruvuma, Simon Maigwa, amesema kuwa bado wanachunguza chanzo kufuatia kifo cha Mwanafunzi wa darasa la sita katika Shule ya Msingi Mtumbatimaji, anayedaiwa kufariki baada ya kutoa mimba.

Kamanda Polisi Mkoa wa Ruvuma, Simon Maigwa

Akizungumza na EATV&EA Radio Digital leo Novemba 8, 2019, Kamanda Maigwa amesema kuwa binti huyo alifikishwa hospitalini akiwa tayari anavuja damu, hivyo bado wanafanyia uchunguzi kwa sababu hata mama mzazi wa binti huyo bado hajatoa maelezo ya kina.

"Ni kweli hili tukio limetokea na bado tunachunguza lakini alipelekwa hosptali na wazazi wake akiwa tayari anavuja damu na baada ya kukaa hospitali akiendelea na matibabu akafariki, mama yake wakati anajaribu kuhojiwa alikuwa anazimia sasa ni masuala ya kibindadamu inabidi kumuacha mtu atulie", amesema Kamanda Maigwa.

Aidha Kamanda Maigwa ameongeza kuwa mara baada ya uchunguzi wa tukio hilo kukamilika, Jeshi la Polisi litatoa taarifa ya kina kuhusu kifo hicho.