Jumapili , 20th Jan , 2019

Msanii wa muziki wa Bongo Fleva ambaye pia ni mjasiriamali wa chakula, Zuwena Mohamed 'Shilole' amefunguka kuwa Rais Magufuli amechangia kukamilisha ujenzi wa nyumba yake.

Rais Dkt. Magufuli akiwa na Shilole.

Shilole amesema kuwa moja kati ya pesa alizopata na kuziwekeza katika ujenzi wa nyumba hiyo, zilitokana na kampeni za urais mwaka 2015 wakati wakimnadi mgombea wa chama cha mapinduzi (CCM), ambaye ndiye rais wa sasa Dkt. John Magufuli.

"Nyumba yangu imejengwa na muziki pamoja na kampeni za kumnadi Rais Magufuli, maana tulikuwa tunalipwa na tulilipwa pesa nyingi ndipo niliamua kuwekeza kwenye nyumba yangu", amesema Shilole.

Shilole ameongeza kuwa, "Mimi ni mnyamwezi nimetoka Tabora kuja mjini kutafuta sijaja kuangalia maghorofa ya Dar, nilivyopata ile hela tu nikasema naenda kununua kiwanja moja kwa moja lakini wapo walionunua magari".

Shilole ni miongoni mwa wasanii wa kike waliofanikiwa kumiliki mjengo na kuuonesha kwenye ukurasa wake wa 'Instagram' mwaka uliopita, ambapo amesema kuwa mjengo huo aliujenga kidogo kidogo na unapatikana maeneo ya Majohe, Gongo la mboto jijini Dar es salaam.