Jumatatu , 19th Feb , 2018

Serikali imeagiza Mkandarasi jengo la abiria uwanja wa ndege wa kimataifa wa Songwe uliopo katika Mkoa wa Mbeya, afikishwe Mahakamani kwa kushindwa kukamilisha kwa wakati ujenzi wa jengo la abiria katika uwanja huo.

Maagizo hayo yametolewa na Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Atashasta Ndikiye wakati akifuatilia utekelezaji wa agizo la Waziri wa Wizara hiyo Prof. Makame Mbarawa ambapo aliagiza kampuni ya kiazalendo ya DB Shapriya ikamilike ujenzi kabla ya Januari 31 mwaka huu.

"Tunahitaji miradi ya serikali ambayo inawagusa wananchi ifanyike na imalizike. Tunataka awamu hii tuoneshe kwa vitendo kwamba tunataka kufanya kazi za nchi", amesema Mhandisi Atashasta.

Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi wa viwanja vya ndege vya mikoa, Joseph Nyahende amemweleza Naibu Waziri Ndikiye kuwa mradi huo ambao pia unahusisha ujenzi wa maegesho ya ndege na barabara, ulikuwa na thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 11 na kwamba hadi sasa serikali haidaiwi na mkandarasi, huku mhandisi mshauri wa mradi huo Silanda Dustan akiishauri serikali kutafuta njia mbadala ya kukamilisha kazi hiyo kwa vile mkandarasi wa sasa hana uwezo.

Msikilize hapa chini  Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Atashasta Ndikiye akifafanua baadhi ya mambo.