Jumapili , 24th Jan , 2021

Serikali imepiga marufuku wananchi wa Kanda ya Ziwa kula nyama ya Nguruwe ikiwa ni hatua za kukabiliana na mlipuko wa homa ya nguruwe uliotokea hivi karibuni.

Picha ya mnyama Nguruwe.

Akizungumza na waandishi wa habari Ofisini kwake Jijini Dodoma Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mashimba Ndaki amesema taarifa zilizopo zinaonyesha Homa ya Nguruwe ilianzia kwenye Halmashauri sita  za Kanda ya Ziwa.

Aidha, imewaagiza wakuu wa mikoa, wilaya na wakurugenzi kuhakikisha wanasimamia kikamilifu karantini zilizowekwa kwa ajili ya kutibu nguruwe ambao tayari wameathirika na ugonjwa huo.

Kutokana na uwepo wa Homa ya Nguruwe tumewataka wananchi wa kanda ya ziwa kuacha kula nyama ya nguruwe ilikukabiliana na ugonjwa huu hatari ambao hauna tiba wala kinga, nawaagiza viongozi mnaohusika mikoani na wilayani kuhakikisha mnasiamia karantini zilizowekwa kwa lengo la kuhakikisha kuwa ugonjwa huu hausambai kwenda maeneo mengine na kuleta madhara,”amesema Waziri Ndaki.

Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mashimba Ndaki.

Waziri Ndaki amezitaja halmashauri ambazo hazitaruhusiwa kula nyama ya Nguruwe  kuwa ni Mbogwe, Sengerema, Geita, Misungwi, Kyerwa na Kahama ambazo kwa kiasi kikubwa zimeathirika na ugonjwa huo.

Amesema hadi kufikia Januari 22, 2020 zaidi ya nguruwe 1,500 sawa na asilimia 10 ya nguruwe wote nchini wamepoteza maisha kutokana na ugonjwa huo.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa  Mifugo Prof. Ezron Nonga amesema lengo la kuzuia wananchi kula nyama ya nguruwe ambayo imeathirika na ugonjwa huo ni kudhibiti usienee kwa kasi katika maeneo mengine ambayo bado hayajaathirika.