Jumatatu , 23rd Nov , 2020

Jumla ya wanafunzi wa kidato cha nne 490,103, wamesajiliwa kufanya mitihani ya kumaliza elimu yao ya sekondari, ambayo imeanza kufanyika hii leo na kati yao watahiniwa wa shule 448,164, na watahiniwa wa kujitegemea ni 41,939.

Katibu Mtendaji wa Baraza la Mitihani la Tanzania (NECTA), Dkt. Charles Msonde.

Taarifa hiyo imetolewa na Katibu Mtendaji wa Baraza la Mitihani la Tanzania (NECTA), Dkt. Charles Msonde, na kusema kuwa kati ya watahiniwa wa shule 448,164, waliosajiliwa, wavulana ni 213, 553 sawa na asilimia 47.7, na wasichana ni 234,611, sawa na asilimia 52.3, huku wenye mahitaji maalum ni 893 na kati yao, 425 ni wenye uoni hafifu, 60 ni wasioona, 186 wenye ulemavu wa kusikia na 222 ni wenye ulemavu wa viungo vya mwili.

Aidha Dkt. Msonde, alivitaja vituo ambavyo vimeripotiwa kujipanga kufanya udanganyifu, katika mitihani inayoanza hii leo katika mikoa mbalimbali hapa nchini, ikiwemo shule ya sekondari Itundu, Mpesu, Wenda, Swila, Onicah, Ntonzo, St Marcus na Kipoke zote za mkoani Mbeya.

Shule zingine ni Geita Adventist na Waja Boys za mkoani Geita, Mary Goret, Agape Junior Seminary, Ebenezer Sango, GreenBird, Mema, Oshara, Sanya Juu na Seuta zote za mkoani Kilimanjaro, Fidel Castrol, Shamiani, Madungu zote za kusini Pemba, pamoja na Mwembeni, Morembe, Marshi na Paroma zote za mkoani Mara.

Shule zingine ni za mkoani Ruvuma, Morogoro, Mjini Magharibi, Mwanza, Simiyu, Mtwara na Songwe.