Jumapili , 10th Feb , 2019

Msanii na muigizaji wa sauti nchini, Steve Nyerere amemuomba radhi msanii wa muziki wa Bongo fleva, Ommy Dimpoz kufuatia kauli yake ya kuwa msanii huyo asingeweza kuimba tena kutokana na maradhi yaliyomkabili.

Steve Nyerere Ommy Dimpoz

Kupitia ukurasa wake wa instagram Steve ameandika, "kwanza nichukue fursa hii kumshukuru Mungu, nichukue fursa hii kumuomba radhi ndugu yangu Dimpoz kwa namna alivyopokea kauli yangu niliyoitoa dhidi yake.

"Na zaidi niwaombe radhi Watanzania wote na wapenzi wa sanaa binadamu unapoona umekosea busara inatutaka kukiri kukosea nami nakiri kukosea kutokana na ile kauli yangu kwa Dimpoz.' ameongeza Steve

Ameendelea kusema kuwa kauli aliyoitoa haikuwa na maana ya kumtakia mabaya Dimpoz, bali aliongea kwa kukatishwa tamaa kutokana na taarifa alizokuwa akizipata, na kuwataka watu wasichukulie kwa nia mbaya kauli yake.

"Lakini tufahamu kwamba Mungu hufanya miujiza yake kutokana na sababu fulani, hivyo miujiza ya kumuinua ndugu yetu na kurudi kwenye kazi zake imetokana na imani aliyokuwa nayo Dimpoz kwa muumba wake."

Wakati Ommy Dimpoz akiwa kwenye matibabu Afrika Kusini 2018, Steve Nyerere alshawahi kukaririwa na baadhi ya vyombo vya habari nchini kuwa msanii huyo asingeweza kuimba tena kutokana na maradhi aliyokuwa ameyapata kauli ambayo Ommy Dimpoz aliishangaa baada ya kupata nafuu.