
Mzee Sumaye ambaye aliondoka ndani ya Chama Cha Mapinduzi wakati wa uchaguzi Mkuu 2015 na kuhamia Chadema amesema kwamba kitendo cha kiongozi aliyechaguliwa na wananchi kujiuzulu nafasi yake na kuhamia chama kingine kisha kurudi kugombea tena eneo hilo ni ufisadi.
Mwanasiasa huyo mkongwe ameyasema hayo wakati akizungumza na moja ya kituo cha runinga hapa nchini na kusema kwamba mtu kuhama chama kimoja kwenda kingine haina shida lakini mtu anapohama labda kwa kushawishiwa au kwa sababu za maslai binafsi si sawa.
“Huwezi kutoka mbunge ama diwani kutoka Chadema/CUF ukaingia CCM halafu wakakuteua uende kwenye eneo lile lile, hii ni kuchezea fedha za wananchi kwa sababu ni kodi za wananchi, huo ni usifadi mkubwa. “Kama haya yanayotokea ni kwa sababu ya matumizi ya madaraka ama matumizi ya fedha hili jambo tulikemee sote,” amesema Mzee Sumaye.
Kwa kipindi cha mwaka jana wabunge watatu walijiuzulu na kuhamia vyama vingine, waliojiuzulu ni Lazaro Nyalandu, Maulid Mtulia, Dkt. Godwin Mollel, pia kumekuwa na idadi kubwa ya madiwani wanaohama vyama.