Jumatano , 26th Aug , 2015

Rais Jakaya Kikwete amewataka viongozi wa serikali za mitaa kuhakikisha kuwa wanajenga barabara maeneo ya vijijini ili kuchochea maendeleo katika maeneo ya vijijini na kufungua fursa mbalimbali za kiuchumi zilizoko katika maeneo hayo.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete Akiogea na viongozi wa serikali za Mitaa(TAMISEMI)

Kikwete amesema hayo jana wakati akihutubia mkutano wa viongozi wa serikali za mitaa (TAMISEMI) uliowakutanisha wakuu wa mikoa, wilaya pamoja na wakurugenzi kwa lengo la kuimarisha usimamizi wa ubora wa kazi na barabara endelevu, Rais Kikwete amesema kuwa ujenzi wa barabara vijijini utafungua milango ya maendeleo vijijini na kubadilisha maisha ya watu wengi.

Pia Rais Kikwete amewataka viongozi wa serikali za mitaa kuwa waaminifu katika kusimamia mfuko wa barabara ambao umefikia kiasi cha shilingi bilioni 800 ili mfuko huo uweze kuwahudumia watanzania badala ya kuwanufaisha watu wachache.

Waziri wa TAMISEMI ,Hawa Ghasia amesema kuwa wizara yake imeanzisha idara kamili ya miundombinu ambayo itafanya ukaguzi na kuzuia hasara inayotokana na ujenzi wa barabara chini ya kiwango.

Katibu Mkuu wa Wizara ya TAMISEMI, Jumanne Sagini amesema kuwa Wizara hiyo inakabiliwa na changamoto ya kukosekana kwa rasilimali za kutosha hali inayosababisha viwango duni vya barabara vinavyotokana na kukosekana kwa usimamizi na ukaguzi hivyo kutopata barabara endelevu.