Alhamisi , 10th Oct , 2019

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt John Pombe Magufuli, amewataka askari wa wanyamapori kuzingatia maadili ya kazi yao ili kulinda rasilimali za nchi, huku akisisitiza wale wachache wanaoshirikiana na majangili, wafikishwe mahakamani kwa kesi ya uhujumu uchumi.

Rais Magufuli akiwa na Mwenyekiti wa Bodi ya TANAPA Jenerali Mstaafu George Waitara (kulia).

Rais ameyasema hayo kwenye ziara yake mkoani Katavi alipotembelea hifadhi ya Katavi na kujionea shughuli mbalimbali zinazofanyika hapo pamoja na wanyama waliopo hapo.

'Fanyeni kazi, nyie ndio walinzi wa maliasili zetu, Tanzania sio ya kuchezewa tena, wapo wachache wanaoshirikiana na majambazi, wakipatikana wa namna hiyo wapelekeni mahakamani kwenye uhujumu uchumi na kesi iwe kubwa kabisa', amesema Rais Magufuli.

Aidha Rais Magufuli amesisitiza kuwa ili kuleta ufanisi katika ulinzi wa rasilimali za nchi ndio maana akamteua Jenerali Mstaafu George Waitara kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya TANAPA.

'Hapakuwa na sababu ya kumteua mwanajeshi, huyu ni jenerali, amekuwa mkuu wa majeshi nchi nzima na ndio maana tukaanzisha jeshi Usu la kukabiliana na ujangili, kwahiyo fanyeni kazi', ameeleza Rais.