Jumatatu , 29th Dec , 2014

Tanzania ni miongoni mwa nchi ambazo zimechaguliwa kutekeleza mradi wa utafiti wa miaka mitano unaolenga kupata mbinu sahihi za kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi kwenye maeneo kame.

Mtaalam wa mabadiliko ya tabianchi Bw. Edmund Mabhuye kutoka CCCS.

Akiongea Jijini Dar es Salaam kwenye mkutano wa wadau wa Mazingira, Mkurugenzi wa kituo cha mafunzo ya mabadiliko ya tabianchi cha chuo kikuu cha dar es salaam Prof. Pius Yanda amesema mradi huo ambao pia utatekelezwa katika maendeleo mbalimbali ya nchi ya kenya utasaidia kutambua changamoto za mabadiliko ya tabia nchi kwenye maeneo kame na kutoa mbinu mbadala kwa wananchi kutumia rasilimali zilizopo ikiwemo kilimo, mifugo, wanyamapori na fursa za kibiashara katika kujiletea maendeleo:

Wakiwasilisha mada kwenye mkutano huo baadhi ya wadau akiwemo mtaalam wa mazingira kutoka kituo hicho cha mafunzo ya mabadiliko ya tabia nchi cha chuo kikuu cha Dar es salaam Edmund Mabhuye amesema utafiti wa awali umebaini kuwa mabadiliko ya tabianchi yataendelea kuleta madhara kwa wananchi kwenye mikoa ya nyanda kame na amesisitiza umuhimu wa kutiliwa mkazo kwa wakulima na wafugaji kumilikishwa ardhi kisheria ili waweze kujipangia matumizi na kuiendeleza ardhi yao:

Kwa upande wa Tanzania mikoa itakayonufaika na mradi huo wa utafiti wa miaka mitano uitwao Prise utakaotekelezwa kwenye mikoa ya nyanda kame ni pamoja na Mwanza, Shinyanga, Singida, Dodoma na Manyara.