Alhamisi , 17th Oct , 2019

Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA),limesema litayafanyia kazi maelezo ya msanii Menina Tz, mara baada ya kuzungumza naye kuhusu picha na video zake zisizo na maadili, zilizosambaa mitandaoni hivi karibuni.

Kupitia taarifa iliyotolewa leo Oktoba 17, 2019, kupitia ukurasa wa Instagram wa Katibu Mtendaji Mkuu wa Baraza hilo Godfrey Mngereza, imeeleza kuwa jukumu la video hizo kusambaa lipo katika mamlaka zingine hivyo wao watashughulikia maelezo yake pekee.

BASATA kwa pamoja wamesikiliza maelezo ya msanii Menina Abdulkarim, na nini kilichojitokeza katika sakata zima la kusambaa kwa video na picha zake za utupu kupitia mitandao ya kijamii kwa kuwa suala la kusambaa video na picha za utupu za msanii Menina katika mitandao ya kijamii lipo mikononi mwa mamlaka nyingine, BASATA imeamua kuyafanyia kazi maelezo yake” imeeleza taarifa hiyo.

Siku ya Oktoba 11, 2019,  BASATA walimuita msanii huyo ili kuzungumza naye kiundani zaidi kwa lengo la kujua sababu zilizopelekea picha na video hizo kusambaa ili hali masuala ya faragha hayapaswi kuonekana hadharani.