Jumamosi , 5th Oct , 2019

Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) mkoani Kagera, inaendelea kuwahoji watumishi watatu wa idara ya uvuvi na manunuzi katika Halmashauri ya Wilaya ya Kyerwa, kufuatia tuhuma za kuhujumu mradi.

Mkuu wa TAKUKURU mkoa wa Kagera John Joseph

Akitoa taarifa ya utekelezaji wa kazi za taasisi hiyo katika kipindi cha kuanzia Julai hadi Septemba mwaka huu, Mkuu wa TAKUKURU mkoa wa Kagera John Joseph, amesema kuwa wanawashikilia jumla ya watu 29.

Ameeleza kuwa miongoni mwa hao ni watumishi watatu, ambao walitaka kujipatia fedha shilingi milioni nane kutokana na hujuma katika mradi wa upandikizaji vifaranga vya samaki katika ziwa Rushwa lililoko katika wilaya hiyo.

Mkuu huyo amefafanua kuwa watumishi hao walipaswa kupokea vifaranga 35,000 kutoka kwa mzabuni ambaye hakutaka kumtaja kwa sasa, na badala yake walipokea vifaranga 2,040 tu.