Ijumaa , 12th Mar , 2021

Watu wanne raia wa Tanzania leo Machi 12, 2021, wanafikishwa Mahakamani kwa tuhuma za kusafirisha vinyonga 74 na nyoka sita kutoka Milima ya Usambara mkoani Tanga na kuwauza kwa raia wakigeni na wanyama hao kukamatwa nchini Austria.

Kinyonga

Taarifa hiyo ilitolewa na Waziri wa Maliasili na Utalii Dk. Damas Ndumbaro, imesema kuwa Wizara hiyo kwa kushirikiana na vyombo vya ulinzi na usalama vilifanya uchunguzi kuhusu tukio hilo la usafirishaji wa wanyamapori hao.

"Uchunguzi huo umeonesha kwamba siyo tu vinyonga 74 kama ilivyoripotiwa na vyombo vya habari lakini pia kulikuwa na nyoka sita na uchunguzi umewatia hatiani Watanzania wanne na wamekiri kuwauzia wazungu wawili," ameelezea Dk. Ndumbaro.

Katika hatua nyingine Dk. Ndumbaro, amewataka Watanzania kuwa wazalendo kwa kulinda wanyamapori ili kutoathiri uchumi wa sekta ya utalii kutokana na serikali kusitisha usafirishaji wa wanyamapori hai tangu Mei 2016.