Alhamisi , 15th Dec , 2016

Chama cha waandishi wa habari mkoani Mbeya (MBPC) kimesema hakijaridhishwa na hukumu iliyomwacha huru dereva Herman Joseph (33) aliyekuwa akiendesha gari iliyowagonga na kuwajeruhi wanahabari watatu waliokuwa njiani kuelekea kazini.

Mwenyekiti wa MBPC, Modestus Nkulu

Mnamo Agosti 31 mwaka huu,gari namba T 321 CDA aina ya Toyota Landcruiser mali ya kampuni ya Shanta Mining iliyokuwa ikiendeshwa na Joseph iliwagonga wanahabari Aines Thobias na Gabriel Kandonga na kuwasababishia kila mmoja kuvunjika mguu huku mwenzao Ibrahim Yasin akipata majeraha madogo.

Wanahabari hao watatu walikuwa wakitumia usafiri wa pikipiki wakitokea Mbalizi wilayani Mbeya wakielekea wilayani Songwe walikokuwa wanakwenda kufanya kazi lakini wakiwa njiani waligongwa na gari hiyo na kulazimika kukatisha safari yao.

Shitaka hilo lilifikishwa katika mahakama ya Wilaya ya Mbeya chini ya hakimu mkazi Zawadi Laizer huku wakili wa serikali akiwa ni Catherine Paulokwa lakini juzi mahakama hiyo iliamuru mshitakiwa kuachiwa huru.

Katika kikao chake na waandishi wa habari kilichofanyika hii leo, Mwenyekiti wa MBPC, Modestus Nkulu amesema chama hicho hakijaridhishwa na hukumu hiyo na hiyo kinafanya mazungumzo na wanasheria ili kiweze kukata rufaa.

Amesemaa kutoridhishwa maamuzi ya mahakama ni kutokana na mwenendo wa kesi hiyo kutozingatia masuala muhimu ikiwemo kuwaita walioathiriwa na ajali hiyo ili kwenda kutoa ushahidi wao.