Ijumaa , 9th Dec , 2022

Wananchi wa Kitongoji cha Rutozo kilichopo kata ya Katoro mkoani Geita wamemuondoa madarakani aliyekuwa mwenyekiti wao Joseph Mbishi kwa tuhuma za kuwakamata wanawake na kukaa nao muda mrefu ili wakombolewe na waume zao kwa kigezo cha kukusanya michango ya ujenzi wa shule

Mwenyekiti huyo ametolewa kwenye nafasi yake kwa kura za siri zilizopigwa na wananchi baada ya kushindwa kuhudhuria mkutano ulioitishwa kwa ajili ya kujibu hoja za tuhuma zinazomkabili

"Waliomkubali mzee Mbishi aendelee kuwa mwenyekiti wa kitongoji ni 18, Kura zilizoharibika ni kura nane, kura zilizosema kwamba hapana kwamba asiendelee kuwa mwenyekiti wa kitongoji hiki ni kura 456, kwa mujibu wa utaratibu mzee Mbishi tutamuweka pembeni na tutapata mtu mwingine ambae atateuliwa na ofisi ya kata kwa ajili ya kuja kusimamia shughuli za maendeleo katika kitongoji hiki", alisema Shabani. 

Afisa mtendaji kata ya Katoro Selemani Mahushi anasema mwenyekiti huyo alikuwa anatuhumiwa kwa hoja nne ikiwemo kuuza viwanja vya serikali bila utaratibu maalum.

"Kutumia mtu anaejiita Afisa mazingira kufanya utapeli wa fedha kwa mwamvuli wa kuhamasisha usafi, kukusanya mchango wa ujenzi wa shule kwa kuwakamata wanawake na kukaa nao muda mrefu ili wakombolewe na waume zao na pia kuchukua vitu kama nguo na radio, kushindwa kumaliza mradi  wa ujenzi wa shule mpya Mikakati uliochukua zaidi ya miaka mitatu na wananchi kuona mradi huo unahujumiwa ",aisema Mahushi.

Baada ya zoezi la kumuondoa mwenyekiti kufanikiwa wanannchi wakalazimika kuteua watu watatu ambapo mmojawapo atateuliwa na uongozi wa kata kushikilia nafasi ya uenyekiti wa kitongoji hiko na hapa baadhi ya wananchi wanaelezea sababu za kupinga maamuzi hayo.

"Sababu Rushwa ni nyingi, kuna mtu ambao kwamba , watu watatu wale atakubalika mtu huyu mmoja, lakini yule watakaemkubali nzengo inamkubali hawatamchukua, wataenda kupendekeza kwa yule ambao watamtaka wenyewe, lakini nzengo watakaomtaka hawatakubali na sisi hili hatuwezi, sisi ndio tunatakiwa tukubaliane tuchague wenyewe si watu wale wa mbele", alisema Damas.

"Tunaomba serikali yenye mamlaka iliyoko juu kuanzia mheshimiwa  mkuu wa wilaya na mheshimiwa mkuu wa mkoa watusaidie changamoto hii tuliyonayo Rutozo tunasumbuliwa na siasa, sisi wananchi tumekubali kwa ujumla leo bila siasa yeyote  Ile tukaamua kwamba tunemtoa huyu members tupate kiongozi mwingine ambae ataendana na wananchi",  alisema Nyamhanga.

"Utaratibu wa kupata mwenyekiti wa kitongoji ni kwa mujibu wa sheria maana yake sheria, zinaelekeza kwamba baada ya kutokea hiyo hali uchaguzi kwa baadaena kwa nafasi ya serikali utatangaza na baadae kupata mwenyekiti ambae atakuwa na dhamana ya wananchi lakini kwa sasa kazi iliyopo ni kupata kaimu ambae atasimamia shughuli za maendeleo na swala Zima la ulinzi", alisema Sweya.