Jumanne , 26th Jul , 2016

Wananchi wilayani Ludewa, mkoani wa Njombe, wametakiwa kutunza ardhi na kujiepusha na uuzaji holela wa rasilimali hiyo, ili waweze kunufaika kupitia miradi mikubwa ya Liganga na Mchuchuma ambayo ipo mbioni kuanza mapema mwaka 2017.

Mbunge wa Jimbo la Ludewa, Deo Ngalawa akiongea na Wananchi wa Jimbo lake.

Angalizo hilo limetolewa na Mbunge wa Jimbo la Ludewa, Deo Ngalawa, wakati wa ziara ya kutembelea vijiji na Kata zilizopo katika Tarafa ya Mwambao, ambapo amewataka wazee wa eneo hilo kutouza ardhi kiholela kwa wawekezaji wageni, pia huku akiwatak kuwaelimisha vijana kulinda na kuihifadhi rasimali hiyo .

Amesema, kutokana na uwekezaji huo mkubwa, wageni wengi wataingia katika Mkoa na Wilaya hiyo, huku wengi wao wakitamani kuwekeza katika mwambao mwa ziwa Nyasa, ambapo amewataka kutumia fursa hiyo kuwekeza katika ardhi ili kunufaika na miradi hiyo kiuchumi.

Vijiji vya mwambao mwa ziwa Nyasa, vinarasimali kubwa ya ardhi ambayo bado haijaharibiwa na shughuli za kibinadamu, ambayo kama itatumika ipasavyo ni fursa mojawapo ya kujikwamua kiuchumi kwa siku za usoni.