Jumatatu , 27th Jan , 2020

Kutoka kundi la King's Music anaitwa Official Cheed, amefunguka kuwa aliwahi kuuza simu yake ili kwenda nchini Afrika Kusini kwa ajili ya kutafuta maisha pia ametueleza mkasa ambao aliokutana nao wakati anarudi Tanzania kutoka nchini Kenya.

Picha ya msanii wa kundi la Kings Music, Official Cheed

Official Cheed amesimulia hayo kupitia kipindi cha Planet Bongo ya East Africa Radio, wakati anatoa historia fupi ya maisha yake kabla hajatoka kimuziki.

"Kitu ambacho siwezi kukisahau katika maisha yangu, ni kumpa mtu simu yangu kwenda kuuza laki 1, kisha akaenda kununua vocha za elfu 5 kwenda kuwauzia watu bandarini hadi ikafika milioni 1, ili niweze kuchoma sindano katika hospitali ya mnazi mmoja ambayo ni ya kujikinga na maradhi kwa sababu nilikuwa nasafiri kwenda nchini Afrika Kusini" ameeleza.

Akizungumzia tukio ambalo limewahi kumkuta wakati anatokea Nairobi, Kenya kurejea Tanzania Official Cheed amesema "Kuna kipindi nilikuwa Kenya nikakosa passport ya kurudi, ikanilazimu nipande gari la mizigo ili kunivusha, wakati tulivyofika mpakani wanajeshi wakatusimamisha ili kutukagua, sasa kwa hofu yangu kila abiria alijua kama sina passport, wakati tunashuka konda alinipiga bonge la kofi huku ananiambia nikague gari nikajifanya fundi nikazama chini nikiwa na spana" ameongeza.

Aidha msanii huyo ambaye yupo chini ya Alikiba, ameachia wimbo wake mpya unaoitwa for you ambao amemshirikisha Marioo.