Jumatatu , 31st Aug , 2015

Mashindano ya kucheza ya Dance 100% 2015 ambayo yanaendeshwa na East Africa Television (EATV) na East Africa Radio yamefanyika siku ya jumamosi kwa hatua ya robo fainali, na makundi 10 kufanikiwa kuingia hatua ya nusu fainali.

Mratibu wa Mashindano hayo Happy Shame amesema mashindano hayo yalikuwa magumu kwa upande wa wachezaji, kwani kuna baadhi ya makundi yalishawahi kushiriki miaka ya nyuma hivyo yalikuwa na uzoefu na kuleta ushindani mkubwa.

“Mashindano ya leo kidogo yalikuwa ni magumu kwa upande wa wachezaji, kwa maana kuna wa wachezaji hawa waliofika robo fainali kuna vikundi vingi vilishawahi kushiriki miaka mitatu iliyopita na wakaingia kwenye tano bora, lakini tunashukuru kwamba tumepata makundi kumi ambayo tutaenda nayo nusu fainali ambayo itakuwa tarehe 19/9/ 2015, “ alisema Happy Shame.

Pia Bi shame amewataka washiriki waliofanikiwa kuingia hatua ya nusu fainali kujiandaa vya kutosha na kuongeza ubunifu, ili waweze kukabiliana na ushindani utakaokuwepo na kuonyesha utofauti.

Makundi hayo ambayo yanatarajia kuonyeshana ubabe kwenye hatua ya nusu fainali ni Majokery, Wazawa Crew, The Best, Cute Babies, Best Boys Kaka Zao, The Winners, Team ya Shamba, The WD, Team Makorokocho na Quality Boys.