Jumatano , 30th Jan , 2019

Muigizaji wa filamu wa Marekani na mwanamuziki, Jussie Smolet maarufu kama Jamal, ameshambuliwa na watu ambao hawajatambulika ambao wamemmwagia kemikali iliyopelekea kukimbizwa hospitali.

Tukio hilo limetokea jana usiku nchini Marekani, ambapo msanii huyo alikuwa akipita mtaani, na kuvamiwa na vijana wawili huku wakitamka maneno ya kupinga mapenzi ya jinsia moja, ambayo msanii huyo anajihusisha nayo.

Polisi katika mji wa Chicago wamesema wanaendelea na uchunguzi kwa kuangali camera zote za CCTV zilizopo kwenye mtaa shambulio lilipotokea, lakini mpaka sasa hawajapata chochote kuhusu wahusika hao ambao wanaendelea kuwasaka.

Madaktari wamesema wanafanya uchunguzi wa kemikali aliyomwagiwa Jussie, kuona iwapo ina madhara makubwa kwake.

Jussie ameigiza kwenye tanthilia ya Empire kama Jamal Lyon, akivaa uhusika wa mtoto wa Lucious Lyon ambaye pia anajihusisha na mapenzi ya jinsia moja.