Jumapili , 5th Feb , 2017

Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Nape Nnauye ameingilia kati na kutaka busara itumike katika zoezi la kutaja wasanii wanaohusika na dawa za kulevya linalofanywa na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda

Waziri Nape Nnauye akiwa na Wema Sepetu

Nape ametoa ushauri huo leo Mjini Dodoma wakati akizungumza na wanahabari kuhusu sheria mpya wa huduma za habari, ikiwa ni siku nne tangu mkuu huyo wa mkoa aanze kutaja wahusika wa dawa za kulevya wakiwemo wasanii wa bongo fleva na filamu.

Baadhi ya waliotajwa na kutakiwa kuripoti polisi kwa mahojiano ni pamoja na Vanessa Mdee, Wema Sepetu, Nyandu Toz, Chidi Benz, TID, Tunda, Babuu wa Kitaa n.k

Wema Sepetu (Kushoto) alipokuwa akiwasili katika Kituo Kikuu cha Polisi Dar es Salaam kwa agizo la Paul Makonda

 

Nape baada ya kuulizwa swali na wanahabari kuhusu suala hilo amesema kuwa wizara yake inakiri kuwa tatizo hilo ni kubwa, na ilifikia hatua ya kuwasaidia baadhi ya wasanii kwenda kupata matibabu akiwemo msanii Ray C na kwamba wanaunga mkono jitihada zozote za kupambana na tatizo hilo.

Amesema tatizo lipo kwenye namna ya kuwaadhibu wanaogundulika kutumia dawa za kulevya, kwa maana ya sheria ipi itumike kuwashitaki, lakini pia tatizo lingine ni busara inayotumika kuwataja na kuwakamata watu ambao tayari wamekwisha athirika na dawa kulevya badala ya kuwasaidia.

Ameshauri hatua zinazochukuliwa ziepuke kutoharibu nembo ya biashara aliyojijengea msanii husika kwani ni gharama kubwa kurejesha heshima na jina iwapo itabainika kwamba, msanii huyo hakuhusika na tuhuma za kujihusisha na dawa za kulevya.

Waziri Nape Nnauye

Kwa mtazamo wake nape amesema hilo ni tatizo la jamii nzima, na kushauri jamii yote ya watanzania kushiriki katika kujenga maadili ya watoto.

Msikilize hapa alipokuwa akizungumza na wanahabari, leo mjini Dodoma.