Jumanne , 30th Apr , 2019

Rapa Nikki Mbishi 'Unju' amemtaka rapa wa kundi la Weusi, Nikki wa Pili kuacha kumzungumzia endapo hawezi kumuongelea kwa mazuri kuliko anavyoendelea kumchafulia taswira yake.

Nikki Mbishi na Nikki wa Pili

Nikki Mbishi amelazimika kusema hivyo ikiwa ni baada ya video kadha za mahojiano zilizomuonesha Nikki wa Pili akisema hawezi kufanya kazi na Nikki Mbishi kutokana na kwamba hawana mahusiano mazuri ya kibiashara.

"Hiki kijamaa cha kuitwa Nikki Wapili kila kikiulizwa swali kuhusu mimi lazima kiongee CHOO, as if chenyewe ndio kinafanya biashara bora ya muziki, babu ni hivi kama huwezi kufanya kazi na mimi sema huwezi sio kila siku kujaribu kushawishi watu kuwa mimi ni mtu mbaya kwenye biashara".

Ameongeza, "kama huwezi kuniongelea kwa taswira safi na chanya kwa msimamo na mtazamo wangu basi kausha sio mpaka ushawishi watu kuwa NIKKI MBISHI hafai kwanza wewe ni msemaji wa WEUSI sio wa UNJU".

Katika kauli yake Nikki wa Pili alinukuliwa akisema kwamba kwa mtazamo wake katika wimbo wa Wapoloo hawawezi kufanya remix na Nikki Mbishi kutokana na kutojali mahusiano yake na watu jambo ambalo kibiashara siyo zuri.

Akijibu kauli hiyo Nikki Mbishi amesema, "kwanza kazi zenu huwa hamshirikishi watu ishazoeleka, kwahiyo acha kuchafua jina langu. Jifunze kunyamaza kama huna lolote la kunizungumzia. Naongea na wewe Nikki Wapili maana naona tu interviews zako, oooh UNJU hana mahusiano mazuri na watu, watu au nyie tu?. Utadhani hata mshawahi kufurahi mkiona wengine wanapata nafasi. Halafu ni hivi mi sio msanii wa media ni msanii wa mitaa ambayo haifuatilii hata media wakati mwingine mnaimbia media mi narap kwa ajili ya mitaa".

Baada ya tuhuma hizo, Nikki wa Pili amemjibu Nikki Mbishi, "kitaa kuna watu wazima, watoto, wasichana, wakaka, saloon, migahawa, bajaji, boda, uber, kuna sherehe za birthdays na kadhalika, ukisema unafanya muziki wa kitaa basi upatikane huko, ujadiliwe huko uwe kwenye playlist za huko uzunguke huko hicho ndio kitaa kujidanganya ni kazi rahisi".