Alhamisi , 13th Oct , 2016

Jeshi la polisi nchini limesema halipendelei chama chochote cha siasa nchini na badala yake linachofanya ni kutoa ulinzi wa kuhakikisha usalama wa raia na mali zao upo wakati wote.

Msemaji wa Jeshi la Polisi Tanzania, Advera Bulimba

Hayo yamesemwa na Msemaji wa Jeshi la Polisi Tanzania ACP Advera Bulimba wakati akizungumza na wananchi waliokuwa wakimuuliza maswali katika kipindi cha KIKAANGONI kinachorushwa kupitia ukurasa wa Facebook wa EATV ambapo baadhi ya wananchi walitoa madukuduku yao kuhusu upendeleo kwa baadhi ya vyama vya siasa nchini.

“Jeshi la polisi halina upendeleo kwa chama chochote cha siasa nchini, ndiyo maana kila chama kikizingatia kanuni za kuomba mikutano ya hadhara kinapata ulinzi kutoka jeshi la polisi, hivyo kazi yetu kubwa ni kuhakikisha usalama wa raia na mali zao upo, hivyo tukizuia mkutano wowote ni kwa lengo la kudumisha usalama wa raia na mali zao na kupafanya Tanzania kuwa sehemu salama ya nchi."

Aidha Jeshi la polisi limewataka wananchi kuendelea kutoa taarifa ambazo zitasaidia kuimarisha ulinzi na usalama na taarifa watakazotoa zitachukuliwa maanani na kufanyiwa kazi mara moja, na namba za kutumika ni 111 au 112.