Alhamisi , 10th Sep , 2015

Msanii wa muziki wa kizazi kipya (Bongo Flava) David Ganzi maarufu kwa jina la Young Dee amesema

Msanii wa muziki wa kizazi kipya (Bongo Flava) David Ganzi maarufu kwa jina la Young Dee amesema hali halisi inayoendelea nchini kwa sasa ndiyo imemsukuma kufanya wambo wake mpya unaofanya vizuri kwa sasa, aliomshirikisha msanii wa miondoko ya R&B Ben Pol unaoitwa “Do It”

Young Dee ameyasema hayo alipokuwa akichat moja kwa moja na mashabiki katika kipengele cha Kikaangoni Live, kinachoendeshwa na kituo cha televisheni cha East Africa Television (EATV) na East Africa Radio, kupitia mtandao wa Facebook.

Young Dee amesema kutokana na hali ya kisiasa ilivyo ilimlazimu aandike wimbo ambao utahamasisha vijana kujitokeza kwa wingi siku ya kupiga kura, na kufanya maamuzi ambayo ni haki yao kisiasa.

Akiongelea swala la wasanii wengi kuonekana kushabikia vyama tofauti tofauti vya siasa, Young Dee amesema wasanii nao ni wananchi wa kawaida hivyo wana haki ya kushabikia wanachokiamini, na vile vile kwao imekuwa fursa nzuri kibiashara.

KUHUSU MUZIKI

Msanii Young Dee ambae alianza kufanya muziki akiwa na miaka 8 na akiwa shabiki mkubwa wa msanii wa Marekani Lil Wyne, amesema kwa sasa anafikiria kufanya kolabo na msanii wa Nigeria Patoranking, na pia endapo atafanikiwa kufanya nae kolabo, atatumia mtindo wa mchiriku ambao mara nyingi amekuwa akiutumia kwenye muziki wake.

Young Dee amesema hapa nyumbani anawakubali sana wasanii wa miondoko ya hip hop akimtaja Fid Q, Joh Makini, Noorah na Mr. Blue, na pia anafikiria kufanya kolabo na msanii anayefanya vizuri kimataifa kutoka hapa nyumbani Diamond platnumz.

KUHUSU KASHFA YA MADAWA YA KULEVYA NA MAHUSIANO YAKE.

Akiendelea kufunguka kwa mashabiki wake msanii Young Dee amekanusha taarifa ambazo zilikuwepo ya kwamba anatumia madawa ya kulevya, na kusema hajawahi kutumia madawa ya kulevya pamoja na mihadarati.

Kuhusu kuwa na mahusiano na msanii wa Bongo Movie Elizabeth Michael (Lulu) Young dee amekiri kuwahi kuwa na mahusiano nae baada ya shabiki wake kumuuliza kama kweli aliwahi kuwa na mahusiano na msanii huyo.