Jumamosi , 21st Jan , 2017

Mwanamuziki wa nyimbo za Injili nchini Tanzania Bahati Bukuku amewataka watanzania wote kwa ujumla kuwaombea watu hususani wasanii ambao wametumbukia kwenye matumizi ya dawa za kulevya.

Bahati Bukuku Kikaangoni

Bahati akiwa katika kipindi cha Kikaangoni kupitia ukurasa wa Facebook wa EATV ambacho hufanyika LIVE kila Jumatano saa 8 mchana, Bahati amesema kuwa jamii haipaswi kuwatenga wala kuwanyanyapaa, wala kuwasema vibaya bali inapaswa kuwaombea kwa Mungu, ambaye yeye ndiye atakaye wawezesha kuacha matumizi hayo.

Bahati aliyekuwa akijibu swali la mmoja kati ya watu waliojitokeza kuuliza maswali siku hiyo aliyetaka maoni yake kuhusu nini kifanyike ili kuwasaidia wasanii hao, ambapo alisema kuwa hawezi kuwazungumzia wasanii wanaotumia dawa hizo kuhusu kilichowasibu lakini cha msingi ni kuomba ili na vijana wengine wasiingie kwenye mkumbo huo.

"Tunahitaji sisi kama taifa tuwaombee ili warudi kwenye shughuli zao, tuombe tu na vijana wengine pia wasiingie kwenye hayo matumizi" Alisema Bahati

Chid Banz - Msanii wa hip hop Tanzania

Miongoni mwa wasanii waliotajwa katika siku za karibuni kuathirika na matumizi ya dawa za kulevya ni pamoja na Chid Benz, Young D, Ray C, Nando n.k

Kuhusu yeye kufanya kolabo na wasanii wa bongo fleva, Bahati alisema hana mpango wowote wa kufanya muziki wa kidunia wala kushirikiana (kolabo) na mwanamuziki wa bongo fleva na muziki muziki ambao huwa anasikiliza ni wa injili pekee.

 "Siwezi kufanya kolabo na bongo fleva, ...Mara nyingi huwa nasikiliza gospel tu" alisema Bahati.

Kwa waliotaka kujua kama ni kweli kuwa ana mpango wa kuanzisha kanisa, aliwajibu "Sina mpango wa kufungua kanisa, sijawahi kufikiria na sijafungua, nadhani Mungu hajazungumza na mimi katika hilo, akizungumza nitasimama kwenye media kama hivi na nitasema ili watanzania wajue maono na ndoto  zangu..."

Kuhusu historia yake kwenye Injili, alisema "Nilianza kumtumikia Mungu mwaka 1995 nikiwa darasa la sita, nilivutia na historia za Yesu, nikauona ukweli wake, nikaona nimtumikie"

Bahati anasema alizaliwa mwaka 1981, na kwamba aliolewa lakini ndoa yake haikudumu

Kuhusu muziki wa injili kumuingizia pesa, amesema kazi yake ya nyimbo za injili ina pesa za kutosha na ndiyo maana afya yake inakuwa bora zaidi kila siku. "Zamani nilikuwa mwembamba, sasa hivi nina kilo kama 94, haya yote ni matunda ya kumtumikia MUngu kupitia muziki wa Injili"