Ijumaa , 22nd Mar , 2019

Watu wawili wamekamatwa na wengine wanaendelea kuchunguzwa, kufuatia tukio la kurekodi watu zaidi ya 1600 wakiwa ndani ya vyumba vya hoteli, kwa kuwafungia kamera kinyume na sheria.

Tukio hilo ambalo limetokea huko Korea Kusini, limeelezwa kwamba kuna watu waliwalipa wahudumu wa hoteli ili kufunga kamera za siri ndani ya vyumba 42, ambavyo viko kwenye hoteli 30 ndani ya miji 10 ya nchi hiyo.

Jinsi zilivyowekwa

Kamera hizo zilifichwa kwenye runinga, socket za ukutani na drayer la nywele, zilikuwa zikirekodi matukio yote yaliyokuwa yakiendelea ndani ya vyumba hivyo, na kuyarusha moja kwa moja live kwa watu hao.

Site hiyo ambayo video zilikuwa zikioneshwa ilikuwa na wanachama 4000, 97 kati yao walilipia ada ya dola 44.95 kwa mwezi ambazo ni sawa na zaidi ya laki moja ya Kitanzania, na huku wakiwa na uwezo wa kucheza tena mara baada ya kurushwa.

Polisi nchini humo imesema kati ya mwezi November 2018 hadi mwezi huu, mtandao huo ulikuwa umeshaingiza kiasi cha dola 6,000, ambazo ni zaidi ya milioni 14 za Tanzania.

Tukio hilo limeelezwa kuwa si la kwanza nchini humo, baada ya kuwepo kwa matukio ya aina hiyo mara kwa mara, ambapo kamera zimekuwa zikifungwa hadi kwenye vyoo vya umma.